Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemary Staki Senyamule ameipongeza Halmashauri ya wilaya ya Chamwino kwa kupata hati inayoridhisha (hati safi) kwa miaka minne mfululizo kuanzia mwaka wa fedha 2020/2021 hadi mwaka 2023/2024.
Pongezi hizo zimewasilishwa na Mhe. Janeth Mayanja Mkuu wa wilaya ya Chamwino kupitia hotuba aliyoisoma akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwenye mkutano maalum wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri yawilaya ya Chamwino wa kupitia hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha wa 2023/2024 uliofanyika leo Juni 16, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Halmashauri.
" Mhe. Mwenyekiti naomba nitumie fursa hii kwa idhini yako niipongeze Halmashauri ya wilaya ya Chamwino kwa kupata hati safi za ukaguzi zinazoishia 31 Juni 2024 ambayo inaifanya Halmashauri ya wilaya ya Chamwino kuendelea kupata hati safi tangu mwaka wa fedha 2020/2021 hadi 2023/2024. Kitendo hiki kimeipa heshima Halmashauri na Mkoa kwa ujumla. Hongereni sana kwa kazi kubwa mlioendelea kuifanya. " Alisema Mkuu wa Mkoa.
"Ninaamini mafanikio haya yamekuwepo kutokana na ushirikiano uliokuwepo kati yenu ninyi Waheshimiwa Madiwani, wataalam wa Halmashauri, viongozi na wadau mbalimbali wa Halmashauri. Hivyo nawasihi endeleeni kudumisha ushirikiano huo ili kuiwezesha Halmashauri ya Chamwino kuendelea Kupata hati safi katika kaguzi zote kila mwaka kama ambavyo imekuwa ni utamaduni. Alisema Mkuu wa Mkoa.
Pamoja na pongezi hizo ametoa maelekezo kwa Halmashauri kuhakikisha hoja zote ambazo hazijafungwa kuhakikisha zinajibiwa na kufungwa kwa kuzingatia sheria na maelekezo ya Serikali.
Mkuu wa mkoa pia ameipongeza Halmashauri kwa kukusanya mapato vizuri ambapo hadi kufikia Mei 31, 2025 ilikuwa imekusanya 96% ya mapato na kutoa rai kwa watendaji kuhakikisha wanakusanya mapato kwa asilimia zilizobaki na kuhakikisha miradi inasimamiwa na kukamilika.
" kwa taarifa ya uchambuzi wa ukusanyaji wa mapato iliyofanywa na mkoa taarifa inaonesha kufikia 31Mei, 2025 Halmashauri ya Chamwino imekusanya mapato 96%, hivyo niwapongeze kwa kuvuka malengo ya ukusanyaji. Niendelee kusisitiza kuongeza nguvu ya ukusanyaji naamini kwa muda uliobaki kuna mapato bado hayajakusanywa pamoja na kuongeza kasi ya kusimamia na kukamilisha miradi kwa wiki mbili zilizobaki kufikia Juni 30." Alisema Mkuu wa Mkoa.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri Ndugu Tito P. Mganwa ameahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa, Wahe. Madiwani na Mkaguzi Mkuu wa nje wa hesabu za Serikali yaani 'Chief External Auditor'(CEA).
Nao viongozi wa Chama cha Mapinduziwakiongozwa na Mwenyekiti wa Chama Mhe. George Malima na mwenyekiti wa Chama cha ACT Wazalendo mkoa wa Dodoma Ndugu Yohana Musa wamepongeza kazi nzuri iliyofanywa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, Wahe. Madiwani pamoja na Wataalam wa Halmashauri. Aidha wamewaelekeza Mkurugenzi Mtendaji na Wakuu wa Idara kuhakikisha wanasimamia vema na kwa weledi shughuli zote za Halmashauri kwa kipindi ambacho Madiwani hawatakuwepo.
Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino
Sanduku la posta: 1126 Dodoma
Simu ya Mezani: 026 296 1511
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ded@chamwinodc.go.tz
Hakimiliki©2017 Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino. Haki zote Zimehifadhiwa.