Katika hali ya kuongeza lishe bora kwa Wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino, wito umetolewa kwa wamiliki wa mashine za kusaga nafaka hasa unga wa mahindi na ngano kuhakikisha wanafunga kinyunyizi cha virutubisho katika mashine ili Wananchi waweze kupata chakula chenye virutubisho vya aina mbalimbali.
Wito huo wa kufunga vinyunyizi katika mashine maarufu kama (Dosifiers) ambavyo huwa na vitamini A pamoja na madini umetolewa leo tarehe 26 Mei, 2025 wakati wa kikao cha lishe robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2024-2025 kilichofanya katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri.
Hayo yamekuja kufuatia jitihada za Serikali katika kuimarisha ustawi wa lishe bora kwa Wananchi ili kuondokana na lishe duni na ulaji wa chakula usiozingatia makundi sita ya vyakula.
Aidha, wataalam wamehimizwa kutoa elimu kwa wamiliki wa mashine juu ya umuhimu wa kufunga vinyunyizi vya virutubisho ambavyo hutolewa na kufungwa pasi na malipo na Halmashauri kwa kushirikiana na shirika lisilo la kiserikali la Sanku, pamoja elimu kwa Wananchi kutumia vyakula ambavyo vimewekewa virutubisho.
Akizungumza katika kikao hicho Mwenyekiti wa kikao Ndg. Benjamin Gervas Afisa Tawala Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ambaye alimuwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Mh. Janeth Mayanja alisisitiza utolewaji wa elimu hiyo.
“Tuendelee kutoa elimu ili Wananchi wa chini kabisa ambao hawafahamu umuhimu wa haya masuala waweze kufahamu na waweze kutekeleza yale malengo ambayo tumekuwa tukijiwekea”. Alisema Ndg. Benjamin.
Halikadhalika zoezi la utolewaji wa chakula shuleni kwa Wanafunzi limeendelea kutiliwa mkazo katika kikao hicho ili kuhakikisha Wanafunzi katika shule zote wanapata chakula wakiwa shuleni.
“Kuna ambao wanatoa chakula shuleni asilimia 100 lakini kuna baadhi ya shule zina asilimia 20, naona hapa tujifunze kwa wale wanaofanya vizuri wao wanafanyaje mpaka wanafanikiwa maana Wanachi ni walewale kama ni kilimo wote wanategemea kilimo cha aina ileile sasa wenzetu wamefanyaje wameweza kufanikisha kwa asilimia 100 na wengine tupo nyuma.” Alisema Ndg. Eusebi Kessy Mganga Mkuu Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino.
Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino
Sanduku la posta: 1126 Dodoma
Simu ya Mezani: 026 296 1511
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ded@chamwinodc.go.tz
Hakimiliki©2017 Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino. Haki zote Zimehifadhiwa.