Katika Juhudi za kukijanisha Mkoa wa Dodoma, Mkoa huo kupitia Mkuu wa Mkoa Mh. Rosemary Senyamule umekuwa ukitekeleza kampeni ya “Mti wangu birthday yangu” ambayo uhusisha upandaji wa miti kila mwezi ambapo watu mbalimbali hujitokeza kupanda miti katika siku zao za kuzaliwa.
Hatimaye kwa mwezi Mei, 2025 kampeni hiyo imeadhimishwa kimkoa katika Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino ambapo leo tarehe 22 Mei, 2025 miche ya miti ya matunda 350 imepandwa katika Shule ya Sekondari Ndejembi.
Zoezi la upandaji wa miti hiyo liliongozwa na mgeni rasmi Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Mhe. Janeth Mayanja akiambatana na Mkurugenzi Mtendaji Ndg. Tito Mganwa pamoja na wataalam mbalimbali kutoka Halmashauri ambao kwa pamoja walipanda miti hiyo ikiwemo ya mipera, miembe, michungwa, mipapai na parachichi.
Akizungumza wakati wa utekelezaji wa kampeni hiyo Mkuu wa Wilaya amewataka Wananchi kudumisha utamaduni wa kupanda miti katika siku zao za kuzaliwa ili kurithisha vizazi vijavyo tabia ya kupanda miti.
“Kila mmoja amepata mti wa matunda akapande nyumbani kwake na akienda kupanda anakumbuka mti huu niliupanda siku ya birthday yangu, hata watoto, mama, baba na majirani watasikia huyu anapanda mti kwasababu leo ni siku yake ya kuzaliwa maana yake huo utamaduni utakuwa unaendelea kusambaa kwa watu kuwa siku ya birthday yako unatakiwa kupanda mti”. Alisema DC Mayanja.
Aidha, kampeni hiyo pia ni sehemu ya kuunga mkono maono na juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutanza mazingira na kuwa na Tanzania ya kijani kwa kupanda miti.
Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino
Sanduku la posta: 1126 Dodoma
Simu ya Mezani: 026 296 1511
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ded@chamwinodc.go.tz
Hakimiliki©2017 Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino. Haki zote Zimehifadhiwa.