Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Janeth Mayanja jana Januari 19, 2026 amezindua ‘Jukwaa la Uwezeshaji wanawake kiuchumi la Wilaya ya Chamwino’ na kusema kuwa miongoni mwa malengo ya Jukwaa hilo ni kujenga umoja na ushirikiano miongoni mwa wanawake wa Wilaya ya Chamwino ili kuinuana kiuchumi na hatimaye kuwanufaisha wao na familia zao, jamii, na taifa kwa ujumla.
Ameongeza kuwa Jukwaa hilo ni daraja kwa wanawake kufikia fursa mbalimbali zinazopatikana katika jamii, na amewahimiza wawe jasiri, wabunifu na wenye nidhamu, ili waweze kutumia kikamilifu fursa zinazopatikana katika familia, jamii, mashirika, na taasisi mbalimbali.
Vilevile, amewaahidi kuunga mkono juhudi za jukwaa hilo katika kufikia maendeleo jumuishi na endelevu.
kadhalika, Afisa Maendeleo ya Jamii Wilaya, Zaina Msangi ameeleza kuwa faida nyingine zitakzopatikana kupitia jukwaa hilo ni kuwezesha wanawake wa Wilaya ya Chamwino kuwa na sauti moja katika kupanga na kutekeleza miradi ya maendeleo, kukuza uongozi wa wanawake, kuhamasisha wanawake kushiriki katika nafasi za uongozi, na kujenga usawa wa kijinsia.
Zoezi la uzinduzi wa Jukwaa hilo limefanyika katika Ukumbi Mkuu wa Halmashauri, na limetanguliwa na uchaguzi wa viongozi wake, ambapo Katibu Tawala wa Wilaya ya Chamwino, Ndg. Neema Nyelege amesimamia uchaguzi wa viongozi wanne akiwemo Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti, Katibu na Katibu Msaidizi, pamoja na uteuzi wa wajumbe wawili.
Aidha, wanawake hao pia wamepewa elimu kuhusu Mikopo ya 10%, elimu ya bima ya afya kwa wote, pamoja na uundaji na usajili wa vikundi vya huduma ndogo za fedha.
Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino
Sanduku la posta: 1126 Dodoma
Simu ya Mezani: 026 296 1511
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ded@chamwinodc.go.tz
Hakimiliki©2017 Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino. Haki zote Zimehifadhiwa.